Tuesday, July 17, 2012

SMZ KUIMARISHA VYOMBO VYA USAFIRI

Na Khadija Khamis –Maelezo       

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar inaendelea kuchukua hatua kadhaa za kuimarisha  vyombo vya usafiri ili kuhakikisha kwamba huduma hiyo inaimarika kwa  kupatiwa  vyombo vya kisasa  nchini .
Akijibu suala la Mwakilishi, Asha Abdu Haji nafasi za wanawake huko katika ukumbi wa baraza la wawakilishi Mbweni  aliyetaka kujua hatua gani zinazochukuliwa na Serikali ili kuondoa usumbufu wa usafiri kati ya visiwa vya Unguja na Pemba.
Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano Hamad Masoud Hamad alisema kwa ujumla suala la usafiri kwa Unguja na Pemba limekuwa ni tatizo la muda mrefu kutokana na meli kubwa za serikali kuchakaa na kuharibika mara kwa mara na kusababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi .
Aidha alisema serikali ina nia ya kuruhusu kuwepo kwa  biashara huria kwa kuwapa mwamko wafanyabiashara kuanzisha biashara hiyo lakini inaonekana kuwa bado mwamko huo ni  mdogo  .
 
Waziri huyo alisema kuna baadhi ya wafanyabiashara walionyesha nia ya kukubaliana na Serikali kwa kuanzisha ruti za Unguja na Pemba ingawa kumekuwa na matokeo yasiyoridhisha lakini atahakikisha kuwa huduma ya usafiri inaimarika nchini.
Hamad alieleza kuwa serikali itaendelea kuwashajihisha wafanyabiashara ili kuona umuhimu wa kununua meli mpya na zilizosalama  zaidi kama taratibu za usafiri baharini zinavyoelekeza katika kukabiliana na changamoto zilizojitokeza .
‘’Tukipata meli hizi mpya kubwa na za kisasa changamoto zilizopo zitaondoka’’ alisema Hamad .
Alisema kuwa sababu nyingi  zinazojitokeza na kuleta usumbufu  katika usafiri wa bahari ikiwemo uchakavu wa meli, ubovu, masuala ya kiufundi pamoja na hali ya hewa ambavyo huchangia kuwepo kwa matatizo hayo.
Waziri wa Miundombinu alieleza kwamba serikali inachukuwa hatua za kuondoa usumbufu huo kwa kuhakikisha kwamba  wahusika wote  wanafuata sheria ziliwekwa katika vyombo vya usafiri baharini .
Aidha serikali imetoa wito kwa wafanyabiashara kuwekeza katika vyombo vya usafiri hata hivyo inafanya jitihada ya kupata meli nyengine mpya, ambayo itakuwa kubwa ya kisasa itakayokidhi mahitaji ya huduma za usafiri kati ya Unguja na Pemba.  

No comments:

Post a Comment