Sunday, June 23, 2013

VIONGOZI WA SERIKALI, DINI, VYAMA VYA SIASA WATAKIWA KUHUBIRI AMANI MAJUKWAANI


VIONGOZI  wa Serikali, Dini na Vyama vya Siasa nchini wametakiwa kuondoa tofauti zao na kutumia majukwaa kuhubiri amani na upendo ili kudumisha mshikamano  na utulivu ndani ya jamii.

Rai hiyo imetolewa hivi karibuni na Mchungaji wa Kanisa la Moravian Tanzania Jimbo la Kusini Magharibi Ushirika wa Itiri  Daniel Siame wakati wa ibada ya mazishi ya Ditective Sagenti Christopher Kyendesya  aliyefariki Juni 19 mwaka huu wilayani Kisarawe mkoani Pwani kwa ajali ya Pikipiki.
Mchungaji Siame alisema kuwa Serikali haina dini bali jamii ndiyo inadini mbalimbali zikiwemo za Ukristo, Uislamu na Upagani na kuwaomba viongozi hao pale wanapokutana na wananchi kuhubiri mambo yanayompendeza  Mwenyezi Mungu. 
“Inawezekana kuwa ndani ya dini zetu kuna watu ambao wanamapokeo ya dini tu na siyo kumtangaza Mwenyezi Mungu hivyo basi sisi kama viongozi wa Serikali, Dini na Vyama vya siasa tunakazi kubwa ya kutangaza mambo ya kumpendeza Mwenyezi Mungu na amani na siyo mambo ya uchochezi”, alisema Mchungaji Siame.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro alimshukuru mchungaji huyo kwa kuwahimiza watu wote wakiwemo viongozi na wananchi kuhusu umuhimu wa amani na upendo katika jamii.
Kandoro alisema kuwa ni jukumu lao viongozi wa Serikali, Dini na wanasiasa kutumia lugha ya kuwajenga watanzania ili waone kuwa amani ni silaha ya maisha yao ya kila siku kwani ikivurugika msingi mkubwa wa maisha unaharibika na hakuna hata mmoja atakayefurahi kuona kuwa amani na upendo vinatoweka.
Mke wa Rais Mama Salma Kikwete ni miongoni mwa viongozi mbalimbali waliohudhuria mazishi hayo wakiwemo pia maofisa wa Jeshi la Polisi, wanasiasa, wasomi na  watendaji wa Serikali.

No comments:

Post a Comment