Saturday, July 28, 2012

Watoto zaidi ya 1000 wanufaika na ufadhili wa WAMA


Na Mwandishi Maalum, Abuja 
 Zaidi ya watoto wa kike na wa kiume elfu moja  ambao ni yatima na wanaoishi katika mazingira hatarishi kutoka mikoa yote nchini wamenufaika na  ufadhili wa masomo unaotolewa na Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) iliyopo jijini Dar es Salaam.

Hayo yamesemwa jana na mke wa Rais Mama Salma Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi hiyo wakati akiongea kwenye mkutano wa saba wa wake wa marais wa Afrika uliozungumzia masuala ya amani barani Afrika uliomalizika leo mjini Abuja nchini Nigeria.

Mama Kikwete alisema kuwa kati ya wanafunzi waliopata ufadhili huo 532 wanasoma  elimu ya Sekondari katika shule mbalimbali hapa nchini, 250 wanasoma shule ya Sekondari ya mfano ya wasichana inayomilikiwa na Taasisi hiyo ya WAMA-NAKAYAMA iliyopo Rufiji Mkoani Pwani na wanafunzi 12 wanasoma vyuo vya elimu ya juu.

“Taasisi yangu imejenga Shule ya Sekondari ya kata inayomilikiwa na Serikali ya Nyamisati pamoja na nyumba za walimu ambapo jumla ya wanafunzi 320 wanasoma katika shule hiyo, pia tumeweza kujenga mabweni ya wasichana katika shule mbalimbali za sekondari.

Tumechangia elimu kwa kutoa vitabu milioni moja, madawati, vitanda, magodoro  na kufunga umeme wa jua kwenye baadhi ya shule zisizokuwa na umeme”, alisema Mwenyekiti huyo wa WAMA”, alisema Mwenyekiti huyo wa WAMA.


Kwa upande wa afya, Mama Kikwete alisema kuwa  kwa kushirikiana na Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) wamekuwa wakitumia  kampeni ya mtoto wa mwenzio ni wako mkinge na maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi, ambayo lengo lake kuu ni kupunguza maambuikizi ya ugonjwa huo kwa watoto na vijana.
 
Pia Taasisi hiyo imetoa vifaa mbalimbali vya afya ili kupunguza vifo vya kina mama wajawazito na  watoto katika Zahanati, Vituo vya Afya na Hospitali 71, kutoa elimu kwa jamii kuhusiana na umuhimu wa mpango wa kupunguza maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto (PMTCT)  katika mikoa ya Tabora, Pwani, Kagera, Kigoma  na  Mtwara.

Mama Kikwete alisema, “Tumeweza kuwasaidia na kuwainua wanawake kiuchumi kwa kuwapatia elimu ya ujasiriamali na kutoa msaada wa  kifedha kwa vikundi 89 vya Benki za maendeleo vijijini (VICOBA) na Vikundi vya kuweka Akiba na Kukopa (SACCOs), kutoa mafunzo ya ukulima wa zao la pilipili aina ya Paprika kwa wakulima 134 na kutoa elimu ya ujasiriamali kwa wanawake 400 katika mikoa ya Pwani na Dar es Salaam.

Alimalizia kwa kusema kuwa, Taasisi ya WAMA imeweza kutoa  mafunzo ya ujasiriamali  kwa maafisa maendeleo ya jamii katika mikoa ya Lindi ambao waliweza kuvifundisha vikundi vya wanawake katika maeneo ya vijijini, kutoa mafunzo ya Ukimwi na virutubisho vya mwili kwa wanawake 100 na  usindikaji wa vyakula kwa wanawake 120 katika mikoa ya Arusha na Pwani.

Taasisi ya WAMA ilianzishwa mwaka 2006 huku ikiwa na malengo ya kumuinua mwanamke kiuchumi, kuhakikisha kuwa watoto wa kike wanaotoka katika mazingira hatarishi wanapata elimu na kuimarisha afya ya mama wajawazito na watoto.

No comments:

Post a Comment