Wednesday, August 22, 2012

TENGA AKATAA KUJIUZULU KWA RANGE

Kumekuwepo na taarifa tofauti kuhusu kuanza kwa Ligi Kuu ya Bara ambayo kwa mujibu wa kalenda ya Shughuli za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), inatakiwa kuanza Septemba 01, 2012. Baada ya kikao cha pamoja baina ya TFF na viongozi wa klabu za Ligi Kuu kilichofanyika Jumatatu ya Agosti 20, 2012 kwenye ofisi za TFF, TFF inapenda kutoa ufafanuzi ufuatao:
 
1.   Baada ya kikao cha pamoja baina ya TFF, Kamati ya Ligi na viongozi wa klabu zote za Ligi Kuu, ilionekana kuwa kutokana na kutokamilika kwa mazungumzo baina ya TFF/Kamati ya Ligi na mdhamini wa sasa, yaani Vodacom, mwanzo wa Ligi Kuu unatarajiwa kuwa Septemba 15, 2012. Hii inatokana na ukweli kwamba kukamilika kwa mazungumzo baina ya pande husika, ndio kutatoa picha halisi ya Ligi Kuu ya msimu ujao.
 
2.   Mazungumzo baina ya TFF/Kamati ya Ligi na Vodacom yanatarajiwa kukamilika mwishoni mwa wiki hii kwa kuwa yameshafikia hatua nzuri na hivyo mkataba unaweza kusainiwa wakati wowote baada ya kukamilika kwa mazungumzo hayo.
 
3.   Kukamilika kwa mazungumzo hayo ni muhimu kwa kuwa kutasaidia Ligi Kuu kuanza bila ya matatizo yoyote kwa klabu zinazoshiriki, TFF na Kamati ya Ligi hasa kutokana na ukweli kuwa baadhi ya mambo yatakayokubaliwa yatalazimika kuingizwa kwenye Kanuni za Ligi; yatasaidia upatikanaji wa fedha kwa muda muafaka; upatikanaji wa vifaa kwa muda muafaka na masuala mengine muhimu.
 
4.   Ratiba ya Ligi Kuu sasa inatarajiwa kutangazwa mapema wiki ijayo pamoja na tarehe rasmi ya kuanza kwa Ligi Kuu
 
5.   Kutokana na kusogwezwa mbele kwa tarehe ya kuanza kwa Ligi Kuu, mchezo wa Ngao ya Jamii baina ya mabingwa wa Tanzania Bara na washindi wa pili, nao sasa utapangiwa tarehe nyingine ambayo ni wiki moja kabla ya kuanza kwa Ligi Kuu. Kwa maana hiyo mchezo huo utachezwa katika siku itakayotangazwa baadaye.
 
6.   Kuhusu chombo kitakachoongoza Ligi Kuu, TFF ilitoa mapendekezo ya Kamati ya Utendaji kwa Kamati ya Ligi na baadaye kwa viongozi wa klabu za Ligi Kuu kuhusu muundo wa chombo hicho kulingana na mwongozo wa Katiba ya Shirikisho la Kimataifa la Vyama vya Mpira wa Miguu (FIFA) na Katiba ya TFF na suala hilo kwa sasa linajadiliwa na klabu za Ligi Kuu kwa ajili ya hatua za mwisho.

 
SEMINA KWA AJILI YA MAKAMISHNA, WAAMUZI
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeandaa semina kwa ajili ya makamishna (match commissioners), watathmini wa waamuzi (referees assessors) na waamuzi wa daraja la kwanza (class one) ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Ligi Kuu inayotarajia kuanza baadaye mwezi ujao.
 
Kwa upande wa makamishna na watathmini wa waamuzi, semina itafanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Agosti 29-30 mwaka huu. Washiriki wanatakiwa kujigharamia kwa kila kitu; usafiri, malazi na chakula wawapo kwenye semina.
 
Semina kwa waamuzi itafanyika katika vituo vya Dar es Salaam na Mwanza kuanzia Agosti 31- Septemba 2 mwaka huu. Pia nao watajigharamia kwa kila tu. Waamuzi watakaoshiriki semina hiyo ni ambao hawakushiriki ile iliyofanyika Juni mwaka huu na wale walioshiriki lakini hawakufaulu mtihani wa utimamu wa mwili (physical fitness test).
 
Waamuzi wenye beji za Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) hawashiriki kwa vile wao wamekukuwa wakishiriki semina zao zinazoandaliwa na FIFA kila baada ya miezi mitatu.
 
TENGA AKATAA KUJIUZULU KWA RAGE
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Leodegar Tenga amekataa barua ya kuomba kujiuzulu ya mjumbe wa Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF, Ismail Aden Rage.
 
Rage ambaye pia ni Mwenyekiti wa klabu ya Simba alimuandikia Rais Tenga barua ya kujiuzulu wadhifa huo kwa kile alichosema ‘kamati hiyo kushindwa kwa makusudi kusimamia sheria na kanuni za uendeshaji wa mpira Tanzania zinavyoeleza.’
 
Amekataa ombi hilo kwa maelezo kuwa kama Rage amehisi kuwepo udhaifu wa kutosimamia sheria na kanuni kama inavyotakiwa, ni vyema akaendelea kuwemo kwenye kamati hiyo ili kuisaidia kusimamia sheria na kanuni hizo kama inavyotakiwa badala ya kujiuzulu.
 
“Kutokana na uzoefu na uwezo ambao Rage anao katika uongozi wa mpira wa miguu, ni vyema akautumia kuisaidia kamati kutekeleza wajibu wake kama inavyotakiwa kwa mujibu wa sheria ili kusaidia kusukuma mbele gurudumu za maendeleo ya mpira wa miguu,” amesema Rais Tenga.
 
Pia Rais Tenga amesisitiza kuwa ni muhimu kwa mpira wa miguu kuongozwa kwa kufuata sheria na kanuni zilizopo, rai ambayo imetoa kwa kamati zote za TFF ili kuhakikisha kuwa mpira wa miguu unaongozwa bila kuonea wala kupendelea upande wowote.
 
Rais Tenga amesisitiza kuwa kamati hazina budi kuchukua hatua zinazostahili bila woga pale kanuni zinapotaka hatua kuchukuliwa. Amezitaka kamati zisisite kwa namna yoyote ile kuchukua hatua kwa vile kwa kufanya hivyo, uwezekano wa kutokea upendeleo au uonevu utapungua, hivyo mpira wa miguu kuongozwa kwa sheria na haki.

No comments:

Post a Comment