Tuesday, January 29, 2013

ALICHOSEMA WAZIRI MKUU MTWARA NDIO HIKI

Polisi wakati wa fujo za Mtwara.

Taarifa ikufikie kwamba Waziri mkuu Mizengo Pinda amefanikiwa kutuliza jazba za wakazi wa Mkoa wa Mtwara kwa kuwaeleza kuwa kiwanda cha kusindika gesi ghafi kitajengwa kijijini Madimba mkoani humo ili mabaki yatokanayo na gesi hiyo yatumike kuvutia uwekezaji wa viwanda, hii ikiwa ni kauli tofauti na ya madai ya wakazi hao ambao hasira zao zilichangiwa na taarifa kwamba kiwanda hicho kingejengwa Dar es salaam.

Kwenye mkutano wa majumuisho uliofanyika january 29 2013 Waziri mkuu baada ya kusikiliza madai ya wananchi hao kwa siku mbili mfululizo, amesema hakuna tone la gesi ghafi itakayosafirishwa kwa njia ya bomba.

Namkariri akisema “Imani yangu ni kwamba maelezo yametosheleza, mtakua na kiwanda chenu cha kusindika, mtakua na kiwanda cha kusafisha, mtakua na hayo matawi kadhaa kwa ajili ya uzalishaji wa umeme kwa ajili ya usindikaji wa viwanda”
Mwanzoni madai ya wakazi wa Mtwara yalikua ni kupinga usafirishaji wa gesi ghafi mpaka Dar es salaam wakieleza kwamba huo mpango utafukuza wawekezaji wa viwanda Mtwara ambao ungechochewa na upatikanaji wa malighafi baada ya kusafishwa kwa gesi.
Jengo la Mahakama lililotelekezwa.

Pia wananchi walipinga ujenzi wa mitambo ya kuzalisha umeme kinyerezi Dar es salaam na badala yake wakataka hiyo mitambo ijengwe hukohuko Mtwara.

Kwenye mstari mwingine Waziri Mkuu aliwataka wananchi kumsamehe mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali mstaafu Joseph Simbakalia kwa kauli alizotoa december 21 2012 katika kikao cha kamati ya ushauri pale alipoombwa kuyapokea maandamano ya wakazi wa mkoa huo december 27 ambapo aliwaita wapuuzi na wahaini.

Waziri mkuu katika majumuisho yake aliambatana na Waziri wa Ardhi nyumba na maendeleo ya kazi profesa Anna Tibaijuka, Waziri wa Uchukuzi Dr. Harrison Mwakyembe, Waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi Dr. Shukuru Kawambwa na Waziri wa mambo ya ndani Dr. Emmanuel Nchimbi.

Katika hizo siku mbili pia Waziri mkuu alikutana na vyama vya siasa vya upinzani, chama cha Mapinduzi CCM, viongozi wa dini ya Kiislamu na Kikristo, Wafanyabiashara, Madiwani na wenyeviti wa mitaa pamoja na Wanaharakati.

No comments:

Post a Comment